SERIKALI imetenga jumla ya Sh bilioni 811 zitakazotumika kutekeleza
ahadi ya Rais John Magufuli ya kukipatia kila kijiji Sh milioni 50 kwa
ajili ya shughuli za maendeleo. Imeelezwa kwamba serikali imeshaanza
kushirikisha wadau mbalimbali kupata maoni ya jinsi ya kuendesha mpango
huo kwa ufanisi na tija.
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa ameishukia Idara ya Uhamiaji nchini
akiituhumu kuruhusu uingizaji holela wa wageni mkoani Kagera. Amesema
ongezeko hilo la kiholela la wageni hao ni hatari kwa ustawi wa mkoa na
taifa kwa ujumla.
RAIS John Magufuli amewathibitisha watendaji wakuu wa taasisi mbili
za serikali; ambazo ni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru). Waliothibitishwa ni
Alphayo Kidata, aliyekuwa Kaimu Kamishna Mkuu wa TRA ambaye anakuwa
Kamishna Mkuu wa taasisi hiyo.
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) imesema itapambana na watu
wanaofanya matukio ya hujuma ikiwemo kuharibu huduma za jamii kwa
wananchi. Aidha, watu wawili wanashikiliwa na Polisi kisiwani Pemba kwa
uchunguzi zaidi kutokana na kutuhumiwa kuhusika na uchomaji moto kwa
nyumba za wakazi pamoja na kituo cha afya na tawi la CCM Tibirinzi.
SERIKALI imesema itatumia ripoti ya Maendeleo ya Binadamu ya mwaka
2015 kama rasilimali muhimu katika kuboresha sera, mikakati na hatua
mbalimbali kuhusu masuala ya kazi ikiwa ni katika kuleta maendeleo.
SERIKALI imeendelea kuwasisitiza Watanzania walionufaika kwa mikopo
ya elimu ya juu kurejesha fedha walizokopa ili wengine wanufaishwe nayo
pia. Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce
Ndalichako alisisitiza hivyo hivi karibuni, alipokuwa akizungumza na
Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha St Joseph cha Dar es Salaam waliogoma
kuingia darasani kwa sababu mbalimbali.
MKUU wa Wilaya ya Temeke, Sophia Mjema amewataka walimu wa wilaya
hiyo kuwa wabunifu ili kutatua baadhi ya matatizo wanayoweza
kuyashughulikia, badala ya kusubiri msaada kutoka kwenye taasisi binafsi
au Serikalini.
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa ameitaka wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera
kudhibiti usafirishaji haramu wa madini ya bati, akieleza kuwa yuko
mwanamke ambaye si rais wa Tanzania anayesafirisha kinyume cha
utaratibu.
MKUU wa Wilaya ya Mvomero, mkoani Morogoro, Betty Mkwasa, amemwagiza
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, kuchukua hatua za
haraka kwa watumishi waliosababisha jengo la vyumba vitatu vya madarasa
katika Shule ya Sekondari Wami kushindwa kutumika.
No comments:
Post a Comment